SOMO # 13: FURAHA ISIYO NA UKOMO


Heri ya mwaka mpya Wapendwa!

Wapendwa siku zote katika Maisha haya tunayoishi hapa duniani wakati mwingine huwa tunapitia changamoto nyingi sana mpaka zinapelekea kukosa furaha kwa kipindi furani, baada ya kusahau furaha hurudi tena. Lakini siku ya leo Mungu anatuambia katika kitabu cha 1 Wathesalonike 5:16 kwamba;- Furahini siku zote.

 

Neno hilo ‘Furahini siku zote’ lina maana kubwa sana katika Maisha yetu endapo kama tutalichukulia kwa uzito mkubwa sana. Mungu kusema hivyo sio kwamba hajui kama huwa wakati mwingine tunapata changamoto ambazo zinatuondolea furaha. Lakini Yeye anatamani tuzichukulie hizo changamoto kama ni sehemu ya Maisha kwani huwa zinamwisho kwahiyo zisituondolee furaha ndani ya mioyo yetu.

 

Mpendwa tambua kwamba Unapokuwa na Yesu kisawasawa ndani yako na ukapata changamoto inatakiwa usiiangalie hiyo changamoto maana itakuondolea furaha bali mwangalie Yesu ,yeye ndio ataiangalia hiyo changamoto na kuindoa huku wewe ukiwa unaendekea kuwa na furaha.  Wakati mwingine inaweza ikawa ni vigumu lakini inaweza ikawa rahisi kama Roho Mtakatifu yupo ndani yako. Roho Mtakatifu ndio huwa anatoa nguvu ya ziada juu ya jambo fulani mpaka kupelekea watu wanaokutazama wasielewe nini kinaendelea kwako.

 

MUHIMU: Furaha isiyo na kikomo kuwa inaambatana na Yesu kuwa ndani yako maana yeye ndio atakufanya uchukuliane na mambo mbalimbali ambayo yanaweza kukuondolea furaha, ndio maana katika kitabu cha Wafilipi 4:4 imeandikwa; Furahini katika Bwana siku zote tena nasema furahini.

 

NINI HUTOKEA FURAHA IKIKOSEKANA?

Furaha inapokosekana ndani ya mtu, maana yake anaweza kufanya mambo mabaya ambapo ndani ya mambo hayo Mungu huwa hayupo kabisa , Yesu huwa hakai mahali ambapo hakuna furaha, ndio maana amesema furahini katika Bwana.

 

Baadhi ya Mambo yafuatayo yanaweza kutokea mtu akakosa furaha;

 

Mtu anaweza asisamehe kabisa au akasamehe baada ya muda mrefu kupita .  Hii ni kwa sababu hana furaha ndani yake juu ya jambo lililomkwaza.

 

Huleta uchungu ndani na moyo. Usipo ruhusu furaha itawale ndani yako maana yake utaendelea kuumia juu ya jambo fulani ambalo limekutokea, na mwisho wake ukawa mabaya.

 

Husababisha kulipiza kisasi. Unapolipiza kisasi maana yake huna furaha ndani yako juu ya huyo mtu , Biblia inasema kisasi ni juu ya Bwana, kwahiyo unapolipiza kisasi umejipa jukumu ambalo sio lako ambapo baadaye itakugharimu tu ndio maana katika kitabu cha Warumi 12:19 imeandikwa; Wapenzi, msijilipize kisasi, bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana imeandikwa, Kisasi ni juu yangu mimi; mimi nitalipa, anena Bwana.

 

Huondoa utu na upendo ndani ya mtu. Furaha ikikosekana ndani ya mtu husababisha mtu huyo wakati mwingine kukosa utu kabisa. Mfano yeye anaona kuuwa ni kawaida tu au kuiba ni kawaida tu kumbe ni kosa mbele za Bwana.

 

Husababisha mtu kujitenga na kuwa ki-vyake vyake tu. Unapojitenga yaani hutaki kuchangamana na watu wengine maana yake wewe huna furaha ndani ya moyo wako, kwahiyo unaona bora ujitenge tu kumbe ndio unajisababishia matatizo zaidi kama ilivyoandikwa katika kitabu cha Mithali 18:1 kwamba; Ajitengaye na wenzake hutafuta matakwa yake mwenyewe; Hushindana na kila shauri jema.

 

Kuwaza mambo mabaya mabaya. Mtu akikosa furaha hata kuwaza kwake huwa kunabadilika, yaani anaanza kuwaza mambo ambayo hata sio mazuri mbele za Bwana, mwisho wa siku anatenda mambo dhambi.

 

Husababisha kukata tamaa. Mtu anapokata tamaa maana yake hana huraha ndani yake, mwisho wa siku inampelekea kufanya mambo mabaya ambapo ni chukizo mbele za Bwana.

 

Husababisha kujiuwa. Mpendwa mtu anapokosa furaha na akakosa msaada wowote ,mwisho wa siku inaweza hata kupelekea  akajiuwa  kwa kunywa sumu au kujinyonga au kujirusha sehemu yoyote ya hatari.

 

Husababisha ndoa kuvunjika au kulega lega. Wanandoa wakikosa furaha ndani ya ndoa yao inaweza kusababisha ndoa hiyo ikavunjika au ikawa na migogoro isiyoisha, yaani unawaona watu kwa nje wanaishi vizuri kumbe ndani ni hatari tupu.

 

Husababisha mtu kuacha kazi. Kuna mtu unakuta hana furaha kazini labda kutokana na mazingira ya kazi kuwa mabaya au imetokea migogoro au ni mvivu wa kufanya kazi. Mtu wa namna hii kwa sababu hana furaha ndani yake anaweza kuacha kazi, kumbe wakati mwingine inakuwa sio kwamba ametatua tatizo bali ndio inaongeza matatizo zaidi.

 

MUHIMU: Mpendwa kama tulivyoona hapo juu inaonesha kwamba huwa kuna madhara mengi sana yanaweza kumpata mtu endapo atakosa furaha ndani ya moyo wake, hivyo basi kama unausoma ujumbe huu na kuna jambo linakutatiza mpaka limekuondolea furaha hebu tushirikishane ili tuweze kuirudhisha furaha yako kama ilivyokuwa awali. Tambua kwamba hakuna faida yoyote nje ya furaha.

MPENDWA MUNGU AKUBARIKI SANA KWA KUUSOMA UJUMBE HUU.

NAKUTAKIA MAFANIKIO MEMA YA MWAKA HUU MPYA 2023.

©Msufu-Januari  07, 2023 mawasiliano 0763242555 na 0753255132

 

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

SOMO # 03: MAAJABU YA NAMBA SABA

SOMO # 01: ADUI

SOMO # 07: MAOMBI